Gyan, Okwi wapewa kazi maalum simba - KULUNZI FIKRA

Tuesday 5 September 2017

Gyan, Okwi wapewa kazi maalum simba

STRAIKA wa Simba Mghana Nicholas Gyan, aliyesajiliwa msimu huu akitokea klabu ya Ebusua Dwarfs ya Ligi Kuu Ghana, juzi alianza makeke kwa kutupia bao na kulichanganya benchi la ufundi la klabu hiyo.

Benchi hilo linakuna kichwa kuhakikisha kuwa Mghana huyo na Emmanuel Okwi wanacheza pamoja ili kuzalisha mabao mengi, jambo litakalowaacha nyota wengine nje.

Gyan alifunga bao la tatu wakati Simba ikiifunga Hard Rock ya Pemba mabao 5-0 kwenye mechi ya kirafiki iliyochezwa Uwanja wa Uhuru, jijini Dar es Salaam.

Gyan aliliambia Mwanaspoti kuwa kiu yake ni kuona anafunga kila mechi na anashukuru aliweza kufanya hivyo juzi na ataendelea kufanya hivyo hata katika Ligi Kuu Bara.

“Baada ya kufanya vizuri katika ligi ya nyumbani Ghana, sasa nimekuja Simba ili kuendeleza kasi yangu ya ufungaji, Simba haitajuta kunisajili,” alisema.

Hata hivyo, Kocha Msaidizi wa Simba, Jackson Mayanja, alisema kwa namna Gyan alivyoonyesha uwezo, ni lazima wapangue safu ya ushambuliaji na kuunda kombinesheni mpya kwa nia ya kumpa nafasi sambamba na Okwi.

“Ni straika aliyeonyesha uwezo wa hali ya juu na ametupa kazi ya kurekebisha safu ya ushambuliaji ili kutengeneza kombinesheni itakayoleta manufaa Simba,” alisema.

Kocha Mayanja alisema Gyan ni straika ambaye walikuwa wakimsaka kwa muda mrefu na kupatikana kwake ni wazi mashabiki wa klabu hiyo watasuuzika nyoyo zao.

Mpaka anaondoka Ghana, Gyan alikuwa wa tatu kwa kufumania nyavu kwa kufunga mabao 11.

No comments:

Post a Comment

Popular