TFF yatoa onyo kali kwa Msuva,Chirwa na Kaseke - KULUNZI FIKRA

Thursday 31 August 2017

TFF yatoa onyo kali kwa Msuva,Chirwa na Kaseke

 
 Kamati ya Nidhamu ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), imemruhusu kiungo mshambuliaji wa Yanga, Mzambia Obrey Chirwa kuendelea kucheza Ligi Kuu ya soka Tanzania Bara baada ya kumpa onyo kali kwa kosa la kumghasi refa.

Hayo yamefikiwa katika kikao cha kamati hiyo iliyo chini ya Mwenyekiti, Tarimba Abbas jana mjini Dar es Salaam na uamuzi huo unamnufaisha pia kiungo mpya wa Singida United, Deus Kaseke.
Kwa pamoja, wakiwa wachezaji wa Yanga, Chirwa, Kaseke na winga mpya wa Difaa Hassan El- Jadida walimsukuma na kumwangusha refa Ludovic Charles katika mechi namba 236 ya Ligi Kuu iliyokutanisha timu hiyo na wenyeji, Mbao FC walioibuka na ushindi wa 1-0 Uwanja wa CCM Kirumba, jijini Mwanza.

Baada ya mchezo huo, Kamati ya Saa 72 ya Bodi ya Ligi ilipitia matukio mbalimbali na kufikia uamuzi wa kuwasimamisha wasubiri suala lao kusikilizwa na kutolewa uamuzi na Kamati ya Nidhamu ya TFF.
Wachezaji hao walidaiwa kufanya kitendo hicho katika mechi hiyo dhidi ya Mbao FC iliyofanyika Mei 20, 2017 kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijni Mwanza. Uamuzi wa Kamati ya Saa 72 ulizingatia Kanuni ya 9(5) ya Ligi Kuu.

Lakini refa, Ludovic Charles naye alipewa onyo kali kwa kutoumudu mchezo kwa mujibu wa Kanuni ya 38(5) ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti wa Waamuzi.
Akizungumza na Waandishi wa habari kwenye ukumbi wa mikutano wa TFF, Uwanja wa Karume, Dar es Salaam, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Nidhamu, Peter Hella amesema kwamba wachezaji wote wapo huru kuendelea na Ligi Kuu baada ya onyo hilo, lakini wanapaswa kujirekebisha

No comments:

Post a Comment

Popular