Baadhi ya marais wenye elimu kubwa Afrika, Rais Magufuli ashika nafasi ya tano - KULUNZI FIKRA

Wednesday 30 August 2017

Baadhi ya marais wenye elimu kubwa Afrika, Rais Magufuli ashika nafasi ya tano

 Sio tu kwamba wana madaraka makubwa ya kisiasa nchini mwao, bali wana elimu kubwa kwenye fani mbalimbali jambo linalothibithisha usemi wa Kiingereza wa “readers are leaders,” yaani viongozi ni watu wenye hulka ya kusoma sana.

Hii ni orodha ya wakuu wa nchi za Afrika wenye elimu kubwa zaidi. Orodha hii ni kutokana na ukubwa wa elimu ya kila mmoja:

Mfalme Mohammed VI (Morocco)

Huyu ni kiongozi wa kwanza kwenye orodha hii; Mohammed wa sita ni Mfalme wa Morocco aliyeshika nafasi hiyo tangu mwaka 1999.

Alimaliza masomo yake ya elimu ya msingi na sekondari katika Shule ya Kifalme nchini Morocco.

Baadaye alipata shahada yake ya kwanza ya Sheria katika Chuo Kikuu cha Mohammed (V) kilichopo Agdal. Ana cheti Elimu ya Juu kwenye fani ya Sayansi ya Siasa.

Alipata shahada ya uzamivu (PhD.) katika Sheria kutoka Chuo Kikuu cha Nice Sophia Antipolis kilichopo nchini Ufaransa.

Dkt. Peter Mutharika (Malawi)

Dkt. Peter Mutharika ni Rais wa Malawi. Alipata shahada yake ya Sheria kutoka Chuo Kikuu cha London nchini Uingereza na akaendelea na masomo na kupata shahada ya Uzamili (Master) ya Sheria na shahada ya Uzamivu (Ph.D) Sayansi ya Sheria kutoka Chuo Kikuu cha Yale nchini Marekani. Pia, Rais Mutharika ni mtaalamu wa Sheria ya Uchumi wa Kimataifa na Katiba.

Alassane Ouattara (Ivory Coast)

Alassane Dramane Ouattara ni Rais wa Ivory Coast tangu mwaka 2010. Alihitimu shahada ya Sayansi Chuo Kikuu cha Drexel kilichopo Philadelphia jijini Pennsylvania, Marekani. Aliendelea na masomo na kupata shahada zake za Uzamili (Master) na Uzamivu (Ph.D) ya Uchumi kutoka chuo Kikuu cha Pennsylvania nchini Marekani. Mwaka jana alichaguliwa kuongoza muhula wa pili wa miaka mitano.

Dkt. Mulatu Teshome (Ethiopia)

Anakaa kwenye nafasi ya nne katika orodha hii. Dkt. Malatu Teshome amekuwa Rais wa nchi ya Ethiopia tangu Oktoba 7 mwaka 2013 baada ya kuchaguliwa na idadi kubwa ya wabunge. Teshome alisoma nchini China ambapo alipata shahada ya Falsafa ya Siasa ya Uchumi wa Siasa na kisha kupata shahada ya Uzamili na Uzamivu katika Sheria za Kimataifa kutoka Chuo Kikuu cha Peking.

Dkt. John Pombe Magufuli (Tanzania)

Alipata shahada yake ya Sayansi kwenye masomo ya Ualimu kwenye masomo ya Kemia na Hisabati kama masomo yake ya kufundishia kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam mwaka 1988. Pia, alihitimu shahada za Uzamili, mwaka 1994 na Uzamivu mwaka 2009 katika somo la Kemia kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Rais Magufuli alisoma Elimu ya Msingi katika Shule ya Msingi Chato kuanzia mwaka 1967 mpaka 1974 na kwenda Shule ya Seminari ya Katoke iliyopo Biharamulo kuanzia mwaka 1975 mpaka 1977 alipohamia Shule ya Sekondari ya Lake mwaka 1977 na kuhitimu mwaka 1978. Alijiunga Shule ya Sekondari Mkwawa kwa elimu ya juu ya Sekondari mwaka 1979 na kuhitimu mwaka 1981. Mwaka huo huo alijiunga na Chuo cha Elimu Mkwawa na kusomea Diploma ya Elimu ya Sayansi kwenye masomo ya Kemia, Hisabati na Ualimu.

[Dkt. Ameenah Gurib (Mauritius)

Dkt. Ameenah Gurib-Fakim ni mwanamke wa kwanza nchini Mauritius kuwahi kuchaguliwa kuwa Rais wa nchi hiyo. Aliingia madarakani mwaka 2015 akiwa ni Rais wa sita wa Taifa hilo.

Alihamia nchini Uingereza na kusoma katika Chuo Kikuu cha Surrey. Alipata shahada ya Sayansi ya Kemia mwaka 1983. Aliendelea na masomo na kupata shahada yake ya Uzamivu ya “Organic Chemistry” kutoka Chuo Kikuu cha Exeter.

Robert Mugabe (Zimbabwe)

Robert Mugabe ameiongoza Zimbabwe tangu nchi hiyo ilipopata Uhuru mwaka 1980. Alianza kwa kuwa Waziri Mkuu kwa miaka saba ya mwanzo, ambapo ilipofika mwaka 1987 mpaka sasa amekuwa ni Rais wa nchi hiyo kwa miaka yote hiyo. Viongozi wa Mataifa ya Magharibi wanasema kwamba Mugabe ni miongoni mwa viongozi makatili zaidi duniani. Lakini ambacho watu wengi hawakijui ni kwamba yeye ni msomi wa hali ya juu pia.
Huu ni muhtasari wa elimu yake: Shahada ya Uzamili ya Sheria (LL.M.), Shahada ya Uzamili ya Sayansi (M.Sc), Shahada ya Elimu (B.Ed), Shahada ya Uongozi (B.A.A) na Shahada ya Sanaa (B.A.)

No comments:

Post a Comment

Popular