Lazaro Nyalandu atoa hotuba nzito baada ya kujiunga rasmi chadema. - KULUNZI FIKRA

Sunday, 19 November 2017

Lazaro Nyalandu atoa hotuba nzito baada ya kujiunga rasmi chadema.

 NASIMAMA mbele yenu na mbele ya Watanzania wote nikiwa nimeisubiri kwa shauku kubwa siku hii ya leo ili nipate fursa ya KUJIUNGA na harakati za kupigania mageuzi ya kisiasa, kijamii, na kiuchumi nchini Tanzania, kwa kujiunga Rasmi na Chama Cha Demokrasia na Maendeleo, Chadema. Asanteni sana kwa upendo wenu na mapokezi makubwa!

Nilijiondoa CCM Oktoba 30 mwaka huu na kujiuzulu nafasi yangu ya Ubunge wa Singida Kaskazini kwa tiketi ya CCM, ikiwa ni pamoja na kujivua nafasi zote za Uongozi ndani ya CCM, ikiwepo Ujumbe wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi, kwa kuwa katika miaka miwili ya Uongozi wa Awamu ya Tano, nimeamini na kujiridhisha kuwa CCM imepoteza mwelekeo, na kwamba niliporejea “Ahadi za Mwanachama wa CCM”, nikakumbushwa maneno haya:

Nitasema KWELI daima, na UONGO kwangu mwiko. Katika Majira na nyakati tunazozipitia kama Taifa,
Na mimi “Naogopa kusema UONGO”. Mabadiliko ya kisiasa ni lazima nchini Tanzania, na Wakati ni huu.

Wakati wa kuondoka CCM, nililijulisha Taifa azma yangu ya kutaka kujiunga na Chadema, endapo Wana Chadema wataona VEMA, kuniruhusu niingie malangoni mwenu. Niwe mmoja wenu, tushikamane pamoja!

Wakati naondoka CCM, nililijulisha TAIFA kuwa, daima nitakuwa mwaminifu kwa nchi yangu Tanzania, na kwamba naungana na Upinzani kupigania HAKI, kwa kuwa imeandikwa HAKI huinua TAIFA, na kwa pamoja tutaitafuta na kuilinda tunu hii muhimu kwa TAIFA letu.

Wakati naondoka CCM, nililijulisha TAIFA kuwa naamini kwamba, Tanzania inahitaji kupata Katiba Mpya, na kwamba tufanye rejea ya RASIMU ya mapendekezo ya Katiba ya Tume ya Warioba ili pamoja na Mambo mengine, kuwepo mgawanyo kamili wa madaraka katika mihilimi ya utawala wa Chini (Bunge, Serikali, na Mahakama), na kuondoa muingiliano na kuweka ukomo wa madaraka wa wazi kwa kila muhimili, ili mwisho wa yote, wenye madaraka kamili ya nchi wabaki kuwa wananchi wenyewe;

Ndugu wana Mwanza,
Nikiwa hapa kuwaomba kura za NDIYO kwa Mgombea UDIWANI wa Chadema kwa Kata hii pendwa,
Naomba kulikumbusha Taifa kuwa katika umoja wetu, tutaishinda hofu, tutaushinda utengano na tutaimarisha demokrasia ya kweli hapa nchini Tanzania.

Na Sasa Saa imefika, na Saa hiyo ndio Sasa, Watanzania tusinung’unike tena, tusiwe na simanzi tena, na tusihuzunike tena, kwa kuwa MUNGU ameruhusu miongoni mwetu, na kwa wote mnaoyasikia MANENO haya, kuamsha mashujaa watakao simama na kuitetea haki Tanzania.

Hakika, Saa imefika ambapo, yeyote ajionaye mnyonge na dhaifu miongoni mwetu na asimama, AKIRI akisema MIMI ni shujaa, kwa kuwa Saa ya mabadiliko inakuja!

Naam, Saa imefika kwa mtu yeyote miongoni mwetu aliye maskini na akiri, MIMI ni tajiri, kwa kuwa ndani yetu, na katika ukiri wetu, tumepewa utayari wa kuiambia Tanzania, MUNGU wako anamiliki. Tumepewa uwezo katika ukiri wetu, wa kubadilisha mwelekeo wa nchi, na kuiambia Tanzania kwamba, wewe nchi ni iliyo chini ya MUNGU Moja, lakini ameruhusu UTAJIRI na Wingi wa mawazo mbadala. Kila Moja wetu, asiogope!

MUNGU Ameruhusu Sasa, Chadema isimame, ikiwa pamoja na vyama vingine vya Upinzania, kama Chama Cha Watanzania wote, bila kujali dini zao, bila kujali makabila yao, na bila kujali mapokeo ya itikadi zao za Kisiasa, ili kuleta mabadiliko mapya ya kiuchumi, kijamii, na kisiasa.

Kwa kuwa imeandikwa katika vitabu zamani, ni “Mizuri kama nini, miguu yao waletayo Habari njema.” Kwa Mwanza, na Tanzania, na kwa wote waliosimama Katika Mkutano huu Mkubwa, tunawatangazia Uhuru kwa wale wasiojisikia huru kuongea, tumekuja kuwatangazia wote walio wapole wa kunena, wasije kunyamaza tena, kwa kuwa SOTE tunaungana kukiri kwa mara nyingine tena, Tanzania bila CCM, inawezekana!

Tuungane pamoja nami, kuwaombeaa afya njema na maisha marefu mpendwa wote wanaopinga mabadiliko, na tuwaombee wana CCM wote Afya njema na maisha marefu, ili kwamba;
MUNGU atakapouinua upinzania na kuibariki tena Tanzania, WAJIONEE wenyewe.
Wakati na hatimaye Tanzania itapopata Katiba Mpya inayolinda haki ya kila mtu, WAJIONEE wenyewe;

Wapinzani watakapo shika dola na kurejesha tena uhuru wa BUNGE, HAKI na DEMOKRASIA katika TAIFA,
WAJIONEE WENYEWE,

Wapinzani wakiwa Ikulu watakapo ruhusu haki ya msingi ya watu kukusanyika, kufanya mikutano ya kisiasa kama wapendavyo, Wakati huo CCM ikiwa ndio Chama Cha Upinzania Bungeni, WAJIONEE wenyewe.

Nimekuja mbele yenu, nisimame miongoni mwenu nikiwa nimeachana na maslahi na heshima yangu ya kuwa Mbunge, niungane nanyi katika harakati za kuleta mabadiliko mapya. Tutasimama pamoja, tutashida pamoja, tutakwea katika mbio za kuwaunganisha Watanzania wote pamoja, na tukuwa daima, TAIFA Moja, Tanzania.

Nimesimama mbele yenu kumnadi Mgombea wa Chadema. Nimepe moyo Shemeji yetu na watoto, na
Nawaomba na nawasisihi, SOTE Tuipe Chadema Kura zote za ndio katika uchaguzi wa udiwani kata hii, na kwingineko nchini katika uchaguzi wa Tarehe Novemba 26.

MUNGU ibariki Tanzania.

No comments:

Post a Comment

Popular