Dr Slaa: kampuni ya stirling ilituhumiwa kwa uzembe buneni - KULUNZI FIKRA

Thursday 24 August 2017

Dr Slaa: kampuni ya stirling ilituhumiwa kwa uzembe buneni

   
 ALIYEKUWA Mbunge wa Karatu na Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Wilbroad Slaa, ameibuka na kudai kwamba kampuni ya ujenzi inayotajwa kuishikilia ndege ya Tanzania aina ya Bombardier Q400-Dash 8, ilikwishatuhumiwa kwa uzembe bungeni.

    Kampuni ya Stirling Civil Engineering Ltd, ndiyo, kwa mujibu wa maelezo ya Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu, imeishikilia ndege hiyo iliyonunuliwa na Tanzania nchini Canada. Uamuzi huo wa kuishikilia unatajwa kuwa ni utekelezaji wa matakwa ya Mahakam a ya Kimataifa ya Usuluhishi, kuiwezesha kampuni hiyo kulipwa deni lake la dhidi ya serikali ya Tanzania la dola za Marekani milioni 38.7 ambazo ni takriban shilingi bilioni 87.

    Msingi wa deni hilo ni kuvunjwa kwa mkataba wa kati ya serikali na kampuni hiyo wa ujenzi wa barabara kutoka eneo la Wazo Hill jijini Dar es Salaam hadi Bagamoyo, mkoani Pwani.

    Akizungumzia kadhia hiyo Dk. Slaa alisema pamoja na hali hiyo, kampuni ya ujenzi ya Stirling si “nadhifu” katika kazi zake na hata wabunge walikwishailalamikia bungeni mwaka 2005, akisisitiza kuwa, yeye ni kati ya wabunge waliopata kuilalamikia kampuni hiyo.

    Katika mawasiliano yake na gazeti hili, Dk. Slaa aliyepata kuwa mgombea urais kwa tiketi ya Chadema kwenye uchaguzi mkuu wa 2010 alisema; “Siamini kama serikali huwa inavunja mikataba ovyo. Kauli hiyo ni vema ikathibitishwa kwa ushahidi na hasa kuonyesha ni vipengele vipi vya mkataba vimevunjwa au sheria ipi imekiukwa. Si vema kutoa kauli za jumla jumla bila uthibitisho.

    Kauli hiyo ya Slaa inapingana na madai ya Lissu ya hivi karibuni kwamba mkataba kati ya serikali na kampuni hiyo ulivunjwa ovyo, kinyume cha utaratibu na ndio maana, kampuni hiyo imekwenda kushitaki katika Mahakama ya Kimataifa na kushinda kesi.

    Slaa anaeleza zaidi; “Kama ni suala la kushikiliwa Bombardier ninachokumbuka ni kuwa kampuni husika ilishindwa kumaliza ujenzi wa barabara hiyo (Wazo Hill hadi Bagamoyo) katika muda uliotajwa ndani ya mkataba.”

    Alieleza kwamba hata sehemu ambayo kampuni hiyo ilikamilisha kipande cha ujenzi wa barabara, basi, ujenzi huo ulikuwa chini ya kiwango na pale kampuni hiyo ilipopewa muda kurekebisha udhaifu huo ilishindwa kufanya hivyo.

    “Bungeni tulipiga sana kelele kuhusu ucheleweshaji huo na kazi isiyoridhisha. Nilikuwa Mbunge wa Karatu wakati huo na Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni na kumbukumbu ziko kwenye hansard, tatizo watu hawapendi kufanya utafiti,” alisema Slaa.

    Akizungumzia suala la Tanzania kushindwa kesi kwenye Mahakama ya Kimataifa, Dk. Slaa alisema; “..hiyo haina maana ya kuwa kampuni hiyo ilikuwa “absolutely” na haki. Mahakama zinategemea zimeelekea wapi hasa hizi za biashara ya kimataifa ambazo kimsingi zinalinda maslahi ya nchi zao. Hili nililizungumzia sana bungeni hasa kutokana na uzoefu wangu katika Bunge la ACP/EU – Joint Assembly ambalo nilikuwa nikiwalisha Bunge la Tanzania mwaka 1996 hadi 2000 .Tuliitaka serikali yetu ichukue hatua bahati mbaya haikuchukua hatua.”
    

No comments:

Post a Comment

Popular