Waziri mkuu: Kiama kinakuja kwa wanaowapa wanafunzi Mimba. - KULUNZI FIKRA

Thursday 1 March 2018

Waziri mkuu: Kiama kinakuja kwa wanaowapa wanafunzi Mimba.

Waziri Mkuu amesema Serikali ina mpango wa kuifanyia marekebisho sheria ya mtoto kwa kuondoa kipengele cha dhamana kwa watu watakaotuhumiwa kuwapa mimba wanafunzi.

Amesema hatua hiyo inatokana na baadhi ya watuhumiwa hao wanapopewa dhamana kwenda kuzungumza na wazazi au walezi wa binti jambo linalochangia katika kuharibu ushahidi.

Waziri Mkuu amesema hayo alipozungumza na wakazi wa Halmashauri ya Mji wa Nanyamba, mkoani Mtwara wakati wa ziara yake mkoani humo.

“Ni bora wakakaa rumande hadi hukumu itakapotolewa na kama hawatakutwa na hatia watarudi uraiani.

“Aidha, Serikali inatarajia kuipitia upya sheria ya elimu pamoja na sheria ya mtoto ili kuweka masharti ya kumlinda mtoto wa kike hususani kudhibiti mimba kwa wanafunzi,” amesema Waziri Mkuu.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Gelasius Byakanwa amesema Serikali itawachukulia hatua watakaobainika kuwapa watoto wa kike dawa za uzazi wa mpango ili kuwazuia wasipate mimba.

Amesema wanafunzi wa kike katika Halmashauri ya Mji wa Nanyamba wamebainika kuwa wanatumia dawa za kuzuia mimba wakiwa shuleni, hivyo kuwaruhusu kushiriki katika matendo yasiyokuwa ya kimasomo.

“Serikali itafanya msako wa kuwatafuta wote wanaotumia dawa hizo pamoja na wanaowapa na watakaobainika hatua kali zitachukuliwa dhidi yao kwa sababu jambo ni hatari kwa maendeleo ya wanafunzi hao,” amesema.

No comments:

Post a Comment

Popular