Siku 27 za kufa kupona majimbo ya kinondoni na Siha. - KULUNZI FIKRA

Sunday, 21 January 2018

Siku 27 za kufa kupona majimbo ya kinondoni na Siha.

Siku 27 za kampeni za uchaguzi mdogo jimbo la Kinondoni na Siha zinatarajiwa kuwa ‘vita’ baina ya vyama vitatu vikubwa vya siasa; CCM, Chadema na CUF.

Wakati CCM ikitamba kuibuka na ushindi katika majimbo hayo kwa madai kuwa Serikali yake imetekeleza yale iliyoahidi, Chadema imesema haitakubali kuchezewa kama ilivyokuwa katika uchaguzi wa kata 43 wa Novemba 26 mwaka jana.

Changamoto zilizoibuka katika uchaguzi huo wa madiwani zilisababisha vyama vinavyounda Ukawa ambavyo ni Chadema, NLD, CUF na NCCR-Mageuzi kususia uchaguzi mdogo wa ubunge wa Longido, Songea Mjini na Singida Kaskazini uliofanyika Januari 13, uamuzi ambao uliungwa mkono na vyama vingine vya Chaumma na ACT- Wazalendo.

Katibu wa itikadi na uenezi wa CCM, Humphrey Polepole alisema jana kwamba chama hicho tawala kitashinda katika chaguzi hizo huku akitaja sababu mbili; “Tunashughulikia shida za wananchi na tunafanya siasa za maendeleo.”

Alisema CCM imejipanga kushinda na itafanya hivyo kwa sababu ni chama kinachoeleweka zaidi kwa wananchi.

Chadema kwa upande wake, imeshapanga safu mbili kila moja ikiwa na vigogo 15 zitakazoweka kambi katika majimbo hayo.

Ile ya Kinondoni itaongozwa na Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye na ile ya Siha itakuwa chini ya mwenyekiti wa chama hicho Freeman Mbowe.

Vita ya kuwania Jimbo la Kinondoni itashuhudia naibu katibu mkuu wa Chadema (Zanzibar), Salum Mwalimu atakavyopambana na mgombea wa CCM, Maulid Mtulia ambaye alikuwa mbunge wa jimbo hilo kwa tiketi ya CUF kabla ya kuhamia chama hicho Desemba 2, mwaka jana hivyo kupoteza sifa ya kuwa mbunge.

Lakini pia kutakuwa na mpambano mkali kati ya Chadema na mgombea wa CUF, Rajabu Salim Juma anayeungwa mkono na chama hicho unaoongozwa na Profesa Ibrahim Lipumba.

Tayari Jumaa ameilalamikia Chadema kwa uamuzi wake wa kumsimamisha Mwalimu kwa madai kuwa unavunja nguvu ya upinzani kuibuka na ushindi.

Mshikemshike mwingine katika uchaguzi huo utakuwa baina ya CUF upande wa Lipumba ambaye anatambuliwa na Msajili wa Vyama vya Siasa kama mwenyekiti halali wa chama hicho, dhidi ya CUF upande unaomuunga mkono katibu mkuu wa chama hicho, Maalim Seif Sharif Hamad ambao unamuunga mkono mgombea wa Chadema kwa mwavuli wa Ukawa.

No comments:

Post a Comment

Popular