Simba yaapa pointi tatu lazima uwanja wa Taifa - KULUNZI FIKRA

Friday, 15 September 2017

Simba yaapa pointi tatu lazima uwanja wa Taifa

Kocha wa Simba, Jackson Mayanja amesema malengo yao ni kupata pointi tatu dhidi ya Mwadui Jumapili licha ya kwamba watawakosa wachezaji  wao wanne walio majeruhi.
Haruna Niyonzima, Juma Liuzio, Erasto Nyoni na Shomari Kapombe wote watakosekana katika mchezo huo utakaofanyika Jumapili kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Mayanja alisema licha ya kuwakosa wachezaji wao bado hawana wasiwasi kwani wana kikosi kipana ambacho kitawapa matokeo mazuri.

"Mechi na Azam hatukucheza katika kiwango bora sana kwani tulitengeneza nafasi chache za mabao na pia hatuweza kutumia nafasi hizo.
"Hivi sasa tumejipanga kuhakikisha tunafanya vizuri kwenye mchezo dhidi ya Mwadui ili kuweza kurejea kileleni kwenye msimamo wa ligi"alisema Mayanja.

Pia Mayanja amewatuliza mashabiki wanaotaka Jonas Mkude acheze akiwataka wavute subira kwani kiungo huyo ni mchezaji mzuri na wakati wowote ataanza kikosi cha kwanza.
Mashabiki kwenye mitandao ya kijamii wameanzisha neno la 'free Mkude' wakimaanisha Mkude awe huru, wakilitaka benchi la ufundi kumtumia kiungo huyo ambaye amekuwa hapati nafasi ya kucheza mara kwa mara tangu kuanza kwa msimu huu.

"Mkude anafanya mazoezi na wenzake na bado ni mchezaji mwenye kiwango na wakati wowote atacheza sio kwamba makocha wanamchukia au kuna watu wanamchukia ila ni mipango ya benchi la ufundi kulingana na mechi husika," alisema Mayanja.

No comments:

Post a Comment

Popular