Beki Mghana amkamia John Bocco - KULUNZI FIKRA

Thursday 7 September 2017

Beki Mghana amkamia John Bocco

BEKI mtata wa Azam, Yakubu Mohammed ameionya Simba kuwa ikijaribu kumtumia straika John Bocco katika mchezo wao wa keshokutwa Jumamosi, wataambulia patupu na kuondoka na aibu.

Yakubu ambaye ameichezea Azam mechi 14 mpaka sasa huku timu hiyo ikiruhusu mabao mawili tu kwenye mechi hizo, ameliambia Mwanaspoti kuwa wanafahamu Bocco hayuko fiti hivyo akipangwa kwenye mchezo huo itakuwa kazi nyepesi kwao kumzuia.

Beki huyo raia wa Ghana alikwenda mbali na kudai hata mshambuliaji Emmanuel Okwi akicheza kwenye mchezo huo hataweza kufua dafu kwani timu yao ya Azam ndiyo yenye beki bora zaidi Ligi Kuu.

“Hata akicheza Okwi (Emmanuel) hawezi kufanya kitu kikubwa, Azam ina beki makini na imara, siyo rahisi kufungika,” alisema Yakubu ambaye anacheza sambamba na Aggrey Morris na Daniel Amoah kwenye nafasi ya ulinzi.

“Wanaweza wakawa wameshinda saba ama tano lakini hiyo siyo sababu ya sisi kuogopa. Wamezifunga timu nyingine na hii ni Azam, timu imara sana,” alifafanua.

“Akicheza Bocco (John) itakuwa kazi nyepesi zaidi. Tunafahamu kwamba ndiyo ameanza mazoezi wiki hii, hatakuwa fiti kucheza dhidi yetu. Akipangwa Simba watakuwa wamejimaliza wenyewe,” alisema.

Katika hatua nyingine, Azam imepanga kumtumia straika wao Yahya Mohammed kuimaliza Simba itakapotua kwenye Uwanja wao wa Azam Complex, kwa mara ya kwanza.

Mohammed ambaye aliomba kutozungumzia mchezo huo, alifichua kwamba rekodi zake kwa sasa zinakwenda poa kwani amefunga mabao manne katika mechi nne za mwisho alizocheza.

Straika huyo aliyekwenda hewani na kushiba, aliifungia Azam bao pekee la ushindi dhidi ya Ndanda kwenye mechi ya ufunguzi wa Ligi huku akifunga mabao mengine matatu katika mechi tatu za kirafiki jambo ambalo limemfanya kuwa na wastani wa kufunga bao moja kila baada ya dakika 90.

No comments:

Post a Comment

Popular