Bashe: Hakuna Mbunge mwenye uhakika wa maisha - KULUNZI FIKRA

Friday 8 September 2017

Bashe: Hakuna Mbunge mwenye uhakika wa maisha

 
 Mbunge wa Nzega Mjini Hussein Bashe amefunguka na kuomba muongozo wa Spika kuhusu hali ya usalama wa nchi, kwa kuwa matukio ambayo yanaendelea kutokea ya kihalifu hayana hitimisho yake.

Bashe amesema hayo wakati akiomba muongozo ndani ya bunge kwa kumtaka Spika wa bunge Job Ndugai kukubali ombi la kamati ya usalama ya bunge likutane na vyombo vya usalama ili yaweze kupatikana majibu ya matukio yanayoendelea kutokea.

"Mhe. Spika katika taifa letu katika kipindi cha muda mrefu kumekuwa yakitokea matukio mbalimbali ambayo sisi kama wawakilishi wa wananchi tuna wajibu wa kupata taarifa sahihi juu ya muendelezo wa matukio hayo ambayo hayana hitimisho", amesema Bashe.
Pamoja na hayo, Bashe ameendelea kwa kusema "sisi tunawaakilisha Watanzania milioni 50 lakini matukio haya yanayotokea yanaharibu heshima ya taifa letu ningekuomba kama utaridhia na wabunge wataniunga mkono, uitake kamati yako ya ulinzi na usalama ya bunge tukufu ikutane na vyombo vya ulinzi na usalama ili tuweze kupata taarifa kamili juu ya mambo haya yanayoendelea katika taifa letu, ili Watanzania na sisi wabunge tuwe na uhakika kwa sababu hali inavyoendelea hakuna mtu mwenye uhakika na maisha yake ya kesho. Dhamana tuliyopewa sisi dhamana ya kusimamia mali, usalama pamoja na raia wa nchi hii", amesisitiza Bashe.

kwa upande wake Spika wa Bunge Mhe. Job Ndugai amekubali hoja iliyotolewa na mbunge Bashe na kutoa amri ya kwa kamati ya ulinzi na usalama ya bunge iende kukutana ili wapange ni jinsi gani ya kulishughulikia jambo hilo na watakapokuwa tayari kabla bunge kuhairishwa siku ya Ijumaa wiki ijayo warudishe majibu kwa bunge juu ya walichoamua.
Tazama hapa uone mbunge Bashe anavyoendelea kuongelea suala la uhalifu nchini

No comments:

Post a Comment

Popular