Balozi atamani kumpeleka Rais Magufuli Marekani kwa wiki tano - KULUNZI FIKRA

Saturday, 16 September 2017

Balozi atamani kumpeleka Rais Magufuli Marekani kwa wiki tano

 Kaimu Balozi wa Marekani hapa nchini, Dk. Inmi Patterson amesema anatamani kumpeleka Rais John Magufuli katika ziara ya wiki tano nchini mwake.

Kaimu Balozi huyo ameyasema hayo hivi karibuni nyumbani kwake jijini Dar es salaam katika hafla ya kumkaribisha Ofisa mpya wa masuala ya kijamii ubalozini, Brinille Ellis.

"Mwaka 1960 Mwalimu Julius Nyerere alifanya ziara ya wiki tano nchini Marekani katika mpango wa kubadilishana uzoefu wa viongozi... wiki tano ni kipindi kirefu, siyo? Kwa hiyo aliweza kutembelea majiji kadhaa", alisema na kuongeza;

"Natamani ningempeleka Rais (John) Magufuli pia katika ziara ya wiki tano Marekani ili na yeye atembelee maeneo kadhaa", alisema Kaimu Balozi huyo na kuibua kicheko kutoka kwa watu waliohudhuria hafla hiyo.

Dk Patterson ameyasema hayo wakati Rais Magufuli akiwa amemaliza zaidi ya miaka miwili madarakani bila ya kufanya ziara nje ya Afrika. Katika hotuba zake kadhaa, Rais Magufuli amesisitiza kuwa hapendi kusafiri nje ya nchi mara kwa mara kwa sababu bado kuna kazi kubwa anayopaswa kuifanya nyumbani.

Tangu achaguliwe Oktoba mwaka 2015, Rais Magufuli ametembelea nchi za Afrika Mashariki na nje ya hapo amewahi kutembelea Ethiopia tu, Amekuwa akihimiza mabalozi wa Tanzania nje kuzifanya kazi ambazo viongozi wakuu wa nchi wanazifanya wanapofanya ziara katika nchi hizo.

No comments:

Post a Comment

Popular