Serikali: Kila Halmashauri ijenge chumba cha upasuaji ndani ya miezi mitatu kuanzia sasa - KULUNZI FIKRA

Tuesday 22 August 2017

Serikali: Kila Halmashauri ijenge chumba cha upasuaji ndani ya miezi mitatu kuanzia sasa

 
 Serikali imetoa miezi mitatu kwa halmashauri zote nchini kujenga vyumba vya upasuaji kwenye zahanati na vituo vya afya ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma za matibabu.
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dk. Hamis Kigwangalla amesema Rais John Magufuli alishatoa maelekezo kwa nchi nzima kuhakikisha zahanati na vituo vya afya,vinakuwa na huduma za upasuaji.


Dk Kigwangalla pia ametoa mwezi mmoja kwa halmashauri ya Meru wilayani Arumeru, kuhakikisha imefunga mifumo ya kielektroniki kwenye zahanati na vituo vya afya ili kudhibiti upotevu wa mapato.
Amesema Serikali haipo tayari kuona mapato yanaendelea kukusanywa kwa kutumia mfumo wa zamani wa kutumia vitabu.


Amesema lazima vituo vya afya na zahanati ziwe na mashine za vipimo vya magonjwa, na upasuaji mdogo lazima ufanyike ili kupunguza msongamano wa wagonjwa kwenye hospitali za wilaya na mikoa.


"Serikali ipo katika hatua za kuboresha huduma za afya hivyo lazima kituo cha afya na zahanati zifanye uchunguzi wa magonjwa na upasuaji," alisema
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Meru, Christopher Kazeri, amesema halmashauri yake, imejipanga kutekeleza maelekezo hayo kabla ya Desemba mwaka huu.

No comments:

Post a Comment

Popular