Mkuu wa Mkoa agoma kukalia kiti cha Mgeni Rasmi. - KULUNZI FIKRA

Monday 14 May 2018

Mkuu wa Mkoa agoma kukalia kiti cha Mgeni Rasmi.

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Rehema Nchimbi amegoma kukaa eneo alilotengewa mgeni rasmi kwa kile alichodai hawezi kukaa kivulini wakati watoto wanakaa juani.

Tukio hilo limetokea leo, Mei 14, wakati Nchimbi akizindua wiki ya elimu inayofanyika kitaifa wilayani Mkalama mkoani Singida.

Nchimbi amechukua hatua hiyo baada ya kupokea maandamano ya shule mbalimbali wilayani humo na kuona watoto wote wamesimama juani.

"Mimi ni mama, mimi ni mwakilishi wa serikali siwezi kukaa kivulini halafu niwaangalie watoto wako juani kwa hiyo watu wote wa meza kuu tushuke pale kwenye jua,”amesema.

Ameongeza: "Serikali ya awamu ya tano ina upendo na huruma kwa watoto na Watanzania haiwezekani watu wazima wakae kivulini watoto wakae juani."

Baada ya kauli hiyo watendaji, viongozi wa serikali na wadau wa elimu ambao walikuwa wamekaa jukwaani walishuka chini na kuhamishia viti vyao juani.

Katika hafla hiyo Nchimbi alipokea maandamano ya wanafunzi wakiwa na mabango mbalimbali yenye ujumbe kuhusu elimu

Mratibu wa Mtandao wa Elimu, Tenmet, Cathleen Swekwao amesema maadhimisho hayo yamefanyika Mkalama kwa kuwa ni wilaya mpya na mwaka jana ilikuwa miongoni mwa wilaya zilizofanya vibaya kwenye matokeo ya darasa la saba.

No comments:

Post a Comment

Popular