Ushahidi wa kesi inayomkabili mwigizaji wa filamu, Wema Sepetu na wenzake wawili kuhusiana na matumizi ya dawa za kulevya aina ya bangi, bado ni kitendawili baada ya kuzua mvutano mzito katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salam jana.
Wakili wa upande wa washtakiwa, Peter Kibatala na Tundu Lisu, wameupinga ushahidi wa vielelezo ambavyo vimefikishwa mahakamani hapo na afisa kutoka Ofisi ya Mkemia Mkuu kwa madai kuwa kuna baadhi ya vitu vimeonekana katika ushahidi huo ambao awali haukutajwa.
Wakili wa serikali, Constantine Kakula alisema ushahidi huo upo lakini bila kusema kuwa kwenye bahasha, suala lililowapa nguvu upande wa washtakiwa kukataa ushahidi huo.
Mara baada ya Hakimu anayesikiliza kesi hiyo, Thomas Simba kutaka ushahidi utolewe hadharani, wakili wa washtakiwa waliendelea kuupinga ushahidi huo kwa madai kuwa hapo awali wakili wa serikali hakusema wala kuonyesha kielelezo hicho kama ushahidi alioutoa mahakamani hapo ukiwa kwenye bahasha nyekundu.
Kesi hiyo imeahirishwa na itasikilizwa tena Agosti 18, mwaka huu.

No comments:
Post a Comment