Mtatiro: Hatufurahi Tanzania kulipa fidia kwa kodi zetu,tunalaum maamuzi yasiyofuata sheria. - KULUNZI FIKRA

Friday, 18 August 2017

Mtatiro: Hatufurahi Tanzania kulipa fidia kwa kodi zetu,tunalaum maamuzi yasiyofuata sheria.

Nimeona kikampeni kinaenezwa mitandaoni, ati kikiwashutumu baadhi ya watu kuwa wamefurahia uamuzi wa kuzuiliwa ndege ya Bombardier, iliyoko huko Canada ambayo ni mali ya Tanzania, kwa sharti la Tanzania kulipa deni lingine linalotokana na uamuzi wake wa miaka nyuma, wa kuvunja moja ya mikataba ya ujenzi wa barabara dhidi ya kampuni ya kigeni.
Sidhani kama kuna watanzania wanaofurahia hali hiyo, watanzania ndiyo wabeba mizigo wa kodi zote zinazotapanywa kulipa faini na matrilioni au mabilioni ya fedha kila serikali yao inapovunja mikataba iliyoingia yenyewe.

Hao wanaoitwa "wanaofurahi nchi inapopatwa na matatizo kama hayo" wala hakuna waliposema kuwa wanafurahia. Wao wameonya, kuwa kilichotokea kwenye hiyo Bombardier ya Canada ndicho kitatokea kwenye kila jambo ambalo tumelifanya kwa kukiuka mikataba na sheria za kimataifa hasa kwenye biashara.

Yapo mambo ni aibu kukaririshana, wapo watu wanatumia nguvu kubwa sana kuaminisha umma kuwa mapambano yoyote tunayoendesha kulinda uchumi wetu kwa kukiuka mikataba tuliyoingia, eti yana tija kwa taifa.

Watu hao wanajiita wazalendo na wanataka tuwaunge mkono. Yani tuunge mkono Propaganda zao. Ukweli ulioko duniani siku zote ni kwamba ukiingia mkataba wowote wa kibiashara, unautekeleza ulivyo, ikiwa unaonewa kwenye mkataba, zipo njia za kutatua jambo hilo ndani ya mkataba wenyewe, hakuna njia ya mkato.

Watanzania wajifunze sana, kwamba vita ya kiuchumi inapiganwa kwa kufuata taratibu mlizoweka kwenye mikataba mliyosaini. PERIOD, hakuna shortcut!

Kuna watu niliwasikia wakishangilia na kumwambia Rais kuwa "fukuza hao Wachimba Dhahabu wasiosikiliza unachosema", ukweli ni kwamba wawekezaji hao walikaribishwa na serikali yetu, wakaingia mikataba na serikali hii hii. Msidanganye kuwa kuna upenyo wa kuwafukuza mkabaki salama, Tanzania si kisiwa!

Utawafukuza leo, kesho watakupeleka kwenye mahakama mlizokubaliana kwenye mkataba, utaamuriwa uwalipe Trilioni 200 (Bajeti halisi ya Tanzania ya Miaka 10), ukikataa kuzilipa iko njia, utashindwa hata kuagiza matrekta nje nchi, ukiyaagiza yatataifishwa, watapewa wawekezaji hao.

Na ukianza kulipa fedha hizo kama ambavyo itatubidi tuwalipe hawa wa-CANADA, mlipaji siyo John Pombe Magufuli (Rais wetu), Mlipaji siyo CCM, Walipaji si hawa waliongia mkataba. Walipaji wa fedha hizo ni sisi wananchi ambao tunalipa kodi usiku na mchana.

Masuala ya namna hii hayana MONOPOLY (umiliki) wa kuyasemea. Wamiliki na wenye haki ya kupiga kelele ni Walipa Kodi. Na ni hatari kubwa sana kuwaita walipa kodi eti hawana uzalendo, JUST BECAUSE wanahoji mambo ya msingi kuhusu nchi yao.

No comments:

Post a Comment

Popular